JamiiForums
JF Official Account
- Nov 9, 2006
- 6,202
- 5,032
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UZINDUZI WA AWAMU YA 4 YA SHINDANO LA “STORIES OF CHANGE”
UZINDUZI WA AWAMU YA 4 YA SHINDANO LA “STORIES OF CHANGE”
JamiiForums (JF) ni Asasi ya Kiraia yenye Makao Makuu jijini Dar es Salaam. JF inashughulika na Haki za Kidigitali, Demokrasia, Uwajibikaji na Utawala Bora. Vilevile, inaratibu Mtandao wa JamiiForums.com ambao umechangia kuleta mabadiliko chanya katika uchakataji wa taarifa na kuchochea Uhuru wa Kujieleza nchini.
Katika Mpango Mkakati wake wa Miaka 5 (2020-2024), JF ilibuni shindano la ‘Stories of Change’ lilioanza mwaka 2021 na katika Awamu Tatu zilizopita, takribani machapisho 6,000 yaliwasilishwa na wananchi. Miongoni mwa maudhui yaliyowasilishwa, yamechangia kuboresha mifumo ya utoaji huduma katika Sekta ya Umma na Binafsi.
Ikiwa na miaka mingi ya uzoefu katika ushiriki wa wananchi, JF inaelewa thamani ya suluhisho zinazosukumwa na wananchi katika kuchochea mabadiliko chanya. Kauli mbiu ya shindano la mwaka huu, itakuwa "Tanzania Tuitakayo" ikilenga kuhamasisha wananchi kuibua mawazo mbadala ya nini kifanyike kuipata Tanzania iliyo bora zaidi kwa kupendekeza mawazo bunifu yanayoweza kutekelezeka ndani ya miaka 5, 10, 15 hadi 25 ijayo. Shindano hilo litaanza rasmi Mei 1, 2024 na kuisha baada ya miezi 2.
Kwa shindano la mwaka huu JF itashirikiana na Twaweza pamoja na wadau wengine kutoka serikalini, asasi za kiraia, mashirika yasiyo ya kiserikali na makampuni binafsi katika nyanja mbalimbali kama habari, elimu, vijana, wanawake, watoto, makundi maalumu, teknolojia, afya na kadhalika; kwa lengo la kuimarisha ushiriki wa wananchi na utekelezaji wa maoni. Wadau hawa ndio watakaoshiriki mchakato wa kupata na kuwatuza washindi wa kisekta.
Vigezo na masharti ya kushiriki katika shindano hili:
- Mshiriki anatakiwa kutayarisha andiko linaloelezea Tanzania Tuitakayo lenye maono ya kibunifu ambayo yanaweza kutekelezeka ndani ya miaka 5, 10, 15 hadi 25 ijayo katika nyanja mbali mbali mfano; elimu, afya, teknolojia, uchumi, mazingira, miundombinu n.k
- Andiko liwe kwa lugha ya Kiswahili au Kiingereza lenye maneno kuanzia 700 hadi 1,000.
- Matumizi ya picha, video na vielelezo vingine yanaruhusiwa ili kuongeza uzito wa wasilisho. Ikiwa picha/video zilizotumika si za mshiriki, atatakiwa kutaja chanzo.
- Machapisho yanatakiwa kuwa halisi na hayajawahi kuchapishwa sehemu nyingine yoyote. Ubwakuzi (Plagiarism) hautaruhusiwa.
- Maandiko yawasilishwe ndani ya miezi 2 kuanzia Mei 01, 2024 kwenye jukwaa la ‘Stories of Change 2024’.
- Ili kushiriki, LAZIMA mtu awe mwanachama aliyejisajili JamiiForums.com ili kuchapisha andiko lake kwenye jukwaa la shindano la ‘Stories of Change’. Ikiwa sio mwanachama, anapaswa kujiandikisha kwa kufuata kiungo hiki Register
Upatikanaji wa washindi
Jopo la majaji linaloundwa na wadau wetu, litaamua washindi kulingana na vigezo vilivyowekwa. Kura za majaji zitabeba 60% ya ushindi huku kura za wananchi jukwaani zikiwa ni 40% ya ushindi.
Washindi watatangazwa kwenye jukwaa la JamiiForums ‘Stories of Change’ na kurasa rasmi (verified) za JamiiForums katika mitandao ya kijamii ambazo ni X (zamani Twitter), Facebook, Instagram, WhatsApp na Telegram tu.
Tunanawaalika wananchi wote wenye miaka 18 na kuendelea kushiriki katika Shindano hili, ili kutimiza haki yao ya msingi ya kuchangia mawazo katika kujenga Tanzania Tuitakayo.
Zawadi kwa Washindi
Katika Msimu wa Nne, washiriki watashindania kitita cha zaidi ya Tsh Milioni 50.
Soma hapa Vigezo na Masharti SoC 2024 - Vigezo na Masharti ya kushiriki katika Shindano la Stories of Change - 2024
====
Anastazia Rugaba
Twaweza ni asasi ya kiraia inayofanya kazi katika nchini 3 za Africa ikiwa ni Tanzania, Uganda na Kenya. Tunafanya kazi kuhakikisha wananchi wanapaza sauiti zao na zinatiwa manani na serikali zao kuanzia za serikali za mtaa mpaka serikali kuu.
Tunafanya tafiti katika nchi hizi tatu tukishirikiana serikali za mtaa na wananchi kwenye vijiji, kata, mikoa na hata kwenye ngazi ya taifa il kuweza kutengeneza sera, sheria, kanuni na taratibu ambazo zinazowapatia kipaumbele zaidi wananchi.
Lakini pia kiu yetu kubwa ni kuona serikali inatumikia umma ambao ndo wamewaweka madarakani na JamiiForums ni wadau wetu wa kubwa wa muda mrefu ikiwemo hili la Stories of Change
Kulingana na Ibara ya 18 katika katiba ya Tanzania inamruhusu kila Mtanzania kutoa maoni yake kwa uhuru pasipokuzuiliwa ilimradi asitukane. Wote tunaamini kalamu ina nguvu kuliko silaha. Ndio maana tumeandaa shindano hili la Stories of Change ili kusudi kila Mtanzania aweze kutumia haki yake ya kikatiba na wajibu wake. Kwasababu haki huendana na wajibu, hakuna haki isiyokuwa na wajibu.
Lakini watanzania wamekuwa wepesi kudai haki pasipo kutimiza wajibu. Tunataka watanzania tutimize wajibu wetu wa kikatiba wa kuandika mawazo yetu. Kila wazo ulilokuwa nalo lina mshiko kwa sababu kila aliefanikiwa amejipanga.