Mfumo wetu wa mahakama unapaswa kujitathmini

Mathanzua

JF-Expert Member
Jan 4, 2017
16,027
20,946
Machi 2023 Rais Samia Suluhu Hassan aligusia ‘mikopo chechefu’ wakati akipokea taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) 2021/2022. Wengi hawakufahamu ni kitu gani.

Pia, nafikiri hata Rais mwenyewe wakati anazungumza hayo hakupewa taarifa vizuri na wasaidizi wake kwamba hata private banks pia zinateseka kwa kiwango cha kutisha na hii mikopo chechefu.

Tangu kupatikana kwa uhuru, madeni chechefu yamekuwa ni changamoto kwenye sekta zinazotoa huduma za fedha nchini jambo linalosababisha taasisi nyingi za kifedha kushindwa kukua kwa mitaji.

Kwa mujibu wa ripoti ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa mwaka 2020, kiwango cha madeni chechefu kilikuwa ni 9.42% tofauti ya 9.58% kwa mwaka 2019. Kiwango cha juu kuliko kinachoruhusiwa cha 5%

Akiwa, Mkurugenzi Mtendaji CRDB, Dk. Charles Kimei alisema kutengwa kwa zaidi ya TZS 150 bilioni kwa ajili ya mikopo chechefu kuliathiri kwa namna moja au nyingine upatikanaji wa faida wa benki hiyo.

Kilichoathiri faida, CRDB waliweka tengo kubwa la mikopo iliyochechefuka, CRDB walitenga TZS 153 bilioni kwa mikopo chechefu kama wasingetenga wangepata faida ya zaidi ya TZS 200 bilioni

Wafanyabiashara wazito wanadhulumu fedha za mabenki kwa kutumia mahakama. Wanachota akiba ya fedha za wateja. Wanagoma kulipa fedha hizo. Wanakimbilia mahakamani. Mahakama zinabariki.

Mchezo huo umekuwa ukifanywa na aina tatu za kampuni; (1) kampuni za mafuta (oil companies) (2) kampuni za usafirishaji (logistics companies) (3) kampuni za kilimo (agricultural companies)

Katika utawala wa awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli, kampuni nyingi zinazofanya huo mchezo, zilifilisika na kukimbia nje ya nchi. Kampuni nyingine zilishtakiwa na wakurugenzi wake kufungwa.

Wanakopa moja kwa moja ndani ya nchi kisha kutengeneza mgogoro na kugoma kulipa kukimbilia mahakamani na kupewa ushindi wa kesi (BIG BON na NBC deni la TZS 22 bilioni, KOM na TADB na AZANIA)

Wanakopa kwa kampuni za kimataifa zinazojihusisha na mikopo ya kimataifa kufanikisha biashara za kimataifa na kitaifa (hudhaminiwa katika makampuni hayo na benki za ndani kwa kupewa Letter of Credit)

Ni barua kutoka benki inayohakikisha malipo ya mnunuzi kwa muuzaji yatapokelewa kwa wakati na kiasi sahihi. Ikiwa mnunuzi hawezi kufanya malipo, benki italipa kiasi kamili au kilichosalia cha ununuzi.

Kwa maana nyingine, ni ahadi ya kimkataba ya benki ya mnunuzi wa kigeni kulipa mara tu msafirishaji anasafirisha bidhaa na kuwasilisha hati zinazohitajika kwa benki ya msafirishaji kama uthibitisho.

Letters of Credit, zinawalinda exporters na importers, kupata biashara na wateja wapya katika masoko ya nje. Msafirishaji anapata hakikisho la malipo huku akimpa muagizaji masharti ya malipo yanayofaa.

Kampuni inakuwa haina uwezo wa kukopeshwa pesa au bidhaa inayouza, hivyo huishirikisha benki ya ndani kutoa udhamini kwa taasisi za kimataifa kwa kutumia (letter of credit) hupatiwa huduma husika

Kwa kuwa dhamana ya mikopo hiyo ni benki, wafanyabiashara hawa hawarudishi mikopo ya watu na hivyo taasisi za kimataifa kuzifanya benki zilizotoa dhamana kuwalipa fedha hizo. BoT wanafahamu.

Benki hulazimika kulipa mikopo hii kisheria na pindi wanaporudi kwa waliowapa udhamini kwa kutumia letter of credit wanakimbilia mahakamani na huko hupewa hukumu za ushindi (hukumu zinazofanana).

Kitu cha kushangaza sana pia, wafanyabiashara wote hawa wanahudumiwa na wakili mmoja tu maarufu kwa kesi za hivyo hapa nchini, anaitwa FRANK MWALONGO. Ni wakili wa mahakama kuu.

Kampuni zote ambazo zime’ default mikopo katika bank za EQUITY, CRDB, NMB, STANBIC wanatumia kampuni ya APPEX ATTORNEYS na mahakamani wanawakilishwa na Wakili Frank Mwalongo.

Hapa chini nitakupa orodha ya kampuni zilizofanya uhuni huo na kiasi cha fedha ambacho kimechuliwa. Mikopo ya aina hii ndiyo ile mikopo chechefu ambayo inahusika kupandisha deni la TAIFA.

KOM (Kahama Oil Mills Limited); (mali ya MHOJA NKWABI KABALO). KOM wamechukua TZS 40 bilioni Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) na kugoma kulipa kwa kukimbilia mahakamani,

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (Tanzania Agricultural Development Bank – TADB) benki ya wakulima, ilianzishwa chini ya Sheria ya Kampuni, 2002 CAP 212 mnamo Septemba 2012.

KAHAMA OIL MILLS LIMITED wamechukua kutoka AZANIA BANK kiasi cha TZS 70 billion , huku wakichukua TZS 110 bilioni kutoka EQUITY BANK na kukataa kulipa zote kisha kukimbilia mahakamani.

TSN Group (mali ya Farouq Baghoza), kampuni inadaiwa TZS 8 bilioni na kampuni ya mafuta ya HASH ENERGY ambazo imekataa kulipa. Pia imechukua NMB BANK kiasi cha TZS 15 bilioni na kugoma kulipa

TSN Group imekopa TZS 80 bilioni EQUITY BANK katika utaratibu wa kudhaminiwa na letter of credit na baadae kukataa kulipa madeni yake na kisha kukimbilia mahakamani, huko walipewa ushindi.

DELINA GROUP (mali ya Davis Mosha), wamekopa CRDB BANK TZS 4 bilioni na KCB BANK $15 milioni ambapo mkopaji alikimbilia mahakamani na kesi yake kuendeshwa na jaji wa ile kesi ya TSN GROUP.

BIGBON PETROLEUM CO. LTD. Walikopa TZS 22 bilioni NBC BANK wakagoma kulipa. Ni nyakati hizo, baadhi ya mali za kampuni hiyo (nyumba zilizokuwa dhamana) katika maeneo ya Kariakoo ziliwaka moto

Masasi Construction Co. Ltd, B.H.Ladwa Ltd, ZAS Investment Company; Kampuni zinamilikiwa na mtu mmoja wamekopa TZS 22 bilioni EQUITY BANK na kukataa kulipa mkopo kwa kukimbilia mahakamani.

ZAS Investment Co. LTD inadaiwa na EQUITY BANK Tanzania LTD TZS 22 bilioni, zikiwa ni mkopo ambao iliiipatia kampuni hiyo kwa ujenzi wa hoteli kwa nyakati tofauti kuanzia 2017, pamoja na riba.

Mahakama Kuu kanda ya DSM, ilitupilia maombi ya ZAS Investment Co. LTD kutaka kuhamisha kesi kutoka kwa Jaji Edwin Kakolaki kwenda kwa Jaji Butamo Phillip. Wakili wa ZAS ni Frank Mwalongo.

GLOBAL AGENCY Co. LTD (Mali ya Fidelis Bashasha); imekopa kiasi cha TZS 26 bilioni benki ya maendeleo ya kilimo (TADB) na kukopa pia bilioni 14 EQUITY BANK na kote huko imekataa kulipa madeni yake.

STATE OIL (T) Ltd (Nilesh Suchak); wamekopa TZS 7 bilioni CRDB, wakakopa TZS 4 bilioni ABC BANK, wakakopa $26 milioni EQUITY BANK na kukataa kulipa. Wakakimbilia mahakamani. Kesi wameshinda

Continental Reliable Clearing (T) Limited (CRC); (mali ya Abri family Iringa), wamekopa na kukataa kulipa $2 milioni, STANBIC BANK. Pia EXIM BANK $3 milioni na EQUITY BANK $11 milioni (zaidi ya TZS 30 bilioni)

Continental Reliable Clearing (T) Limited (CRC) iko hatarini kufungwa kutokana na shauri lililofunguliwa na EQUITY BANK, Equity Bank (T) LTD na Equity Bank (K) LTD, Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Benki hizo zinaidai Continental Reliable Clearing (T) Limited (CRC) zaidi ya $10.5 milioni na TZS 780.6 milioni. Shauri hilo lipo chini ya Jaji Butemo Phillip. CRC wanawakilishwa na Wakili Frank Mwalongo.

Kwa mujibu wa Wakili wa EQUITY, Shalom Samuel Masakyi, CRC imekimbilia mahakamani kujaribu kuzuia uuzwaji wa dhamana ilizoweka kuchelewesha kulipa madeni ili dhamana hizo zisiuzwe.

Nas Hauliers Ltd; walikopa na kukataa kulipa kiasi cha $16 milioni za EQUITY BANK. Wakakimbilia mahakamani. Nas Hauliers Ltd wakapewa ushindi mahakamani dhidi ya EQUITY BANK (T) Ltd.

Jaji Deo John Nangela aliandika hukumu ndefu ya kurasa 164 19/04/2023 akiwapa ushindi Nas Hauliers Ltd katika COMMERCIAL CASE NO. 105 OF 2021 katika High Court Commercial Division

Nini tafsiri ya mambo yote niliyoelesa hapo juu? Ni kwamba fedha za mitaji ya watu wa hali ya chini zinatumika kunufaisha watu wachache wanaojua kuichezea mahakama. Mahakam ipo mfukoni.

Kwa kesi tajwa tu hapo juu zaidi ya TZS 800 bilioni zimeliwa na watu chini ya 10, kiasi ambacho wangekopeshwa wajasiriamali baada ya mikopo kurejeshwa maelfu ya vijana wangepata mikopo

Pesa za TADB ni pesa za serikali, kuzitafuna kihuni ni kutafuna pesa za umma na huo ni ufisadi kama ufisadi mwingine wowote ule. CAG sijaona akiangazia jambo hilo kabisa katika taarifa yake ya udhibiti na ukaguzi.

Pesa za NBC, CRDB, NMB ni pesa mchanganyiko wa watu binafsi na pesa za serikali hivyo kuzitafuna pesa hizo ni kutafuna pesa za umma. Serikali imeweka pesa za umma katika benki hizo tajwa hapo juu.

Zaidi ya asilimia 95 ya benki ya AZANIA ni mifuko ya hifadhi za jamii hasa NSSF, hivyo kuchukua pesa AZANIA BANK bila kurudisha ni sawa na kutafuna vikokotoo vya wastaafu wa serikali na sekta binafsi

Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ni 3nd largest shareholder wa AZANIA Bank (17.97%) na walichukua pesa za wanachama zaidi ya Sh200 bilioni kununua hisa Azania Bank ambayo haijawahi KUTOA GAWIO

Kwa ujumla mahakama inapaswa ijitathmini upya. Mfumo wa mahakama umeoza, umesheheni rushwa na unapaswa kurekebishwa upya. Kama mahakama zinachezewa hivi, nchi yetu haipo salama kabisa.

Heshima na hadhi ya mahakama inalindwa kwa matendo ya watendaji wa mahakama. Ukirejea hizi kesi, zinachafua hadhi, sifa na taswira ya mahakama. Korido za mahakama zimekuwa vyumba vya rushwa?

BoT lazima wasimame kupitia vitengo vyake kuhakikisha inalinda mitaji ya benki hizi, benki zote mitaji yake ni fedha kidogo kidogo zinazowekwa kama akiba za wananchi mbalimbali ikiwemo maskini.

Kituo cha uwekezaji Tanzania (Tanzania Investment Centre TIC) watazame upya namna gani wanalinda uwekezaji. Hapa kuna benki za nje na ndani ya nchi (EQUITY na KCB ni benki za nje), zimetapeliwa.

Kuwaruhusu hawa wafanyabiashara kutapeli mabilioni ya pesa kutumia mahakama za ndani ni sawa na kufedhehesha sera za uwekezaji ambazo serikali inazunguka huko Duniani kuzitangaza.

JAJI MKUU lazima achukue hatua haraka kusafisha taswira na kulinda hadhi ya mahakama ya Tanzania. Jaji Mkuu ndiye tumemkabidhi mahakama zetu, azisimamie zikitemda haki kwa makundi ya aina zote.

Tuhuma za majaji kulambishwa asali zimekuwa nyingi, tuhuma za majaji kupewa maelekezo na wanasiasa ili kutoa upendeleo zimekuwa zikiongezeka kila siku. Je, JAJI MKUU umeridhika?

Mwisho, kwa kuwa kidole hiki naelekeza katika mhimili muhimu wa kutafsiri sheria na kutoa haki, hivyo, katika hili ni muhimu sana JAJI MKUU mapema utazame wapi panapovuja ukazibe.

Nakala kwa; Rais @SuluhuSamia @ikulumawasliano @mwigulunchemba1 @judiciarytz @InvestTanzania

Mwandishi: Martin Maranja Masese
 
Mahakama wanamambo ya hovyo sana.huwa wanafanya maamuzi ya hovyo Kwa kujificha kwenye kigezo Cha mahakama haiingiliwi.Tz Kila kitu ni hovyo hovyo tu.
 
Back
Top Bottom