Nina swali ndugu zangu hivi inawezekana siku za hatari zikaangukia katika mzunguko kuingiliana na siku za hedhi?
Mfano, siku za hedhi ni tano ile siku ya 4 au 5 ikiwa siku ya hatari?🤔
Mfano, siku za hedhi ni tano ile siku ya 4 au 5 ikiwa siku ya hatari?🤔
- Tunachokijua
- Hedhi ni tendo la kibaiolojia linalotokea kila mwezi kwenye maisha ya mwanamke aliyevunja ungo. Tendo hili huhusisha utoaji wa damu na tishu za mwili kutoka kwenye mji wa uzazi kupitia uke.
Mfumo wa homoni za mwili ndio huongoza mzunguko wa hedhi ya mwanamke. Japokuwa mzunguko huu unaweza kuchukua siku zozote kati ya 21-35, wanawake wengi huwa na mzunguko wa wastani wa siku 28 ambao kwa lugha rahisi hufahamika kama mzunguko wa kawaida.
Katika hali ya kawaida, mzunguko wa hedhi wa kila mwezi hugawanywa kwenye vipindi vinne ambapo kimoja kati yake huitwa Ovulation, yaani kipindi cha utolewaji (uanguaji) wa yai lililopevuka, kipindi ambacho kwa lugha maarufu inayofahamika sana mitaani huitwa kipindi cha siku za hatari.
Kila mzunguko wa hedhi huwa na siku yake ya kutoa yai kwa mwezi husika, siku hii ndio yenye uwezekano mkubwa zaidi wa kupata ujauzito kuliko zingine.
Mathalani, siku ya ovulation kwa mtu mwenye mzunguko wa siku 35 ni tofauti na mwanamke mwenye mzunguko wa siku 28. Hali ipo hivyo kwa mizunguko mingine pia.
Rejea jedwali hili linaloonesha siku za hatari kwa kila mzunguko.
Jedwali la mizunguko ya hedhi (JamiiForums)Kupata mimba wakati wa hedhi
Kama ilivyofafanuliwa awali, kila mzunguko wa hedhi huwa na siku yake ya ovulation ambayo huambatana na siku zingine kadhaa ambao kwazo pia mwanamke anaweza kupata ujauzito.
Kwa hesabu za kawaida, siku hii hutokea wastani wa siku 14 kabla ya kutokea kwa hedhi ya kila mwezi.
Swali linabaki kuwa, inawezekana kwa baadhi ya wanawake kupata mimba huku wakiwa kwenye siku zao za hedhi?
JamiiForums imefuatilia suala hili na kubaini kuwa kisayansi linawezekana. Mathalani, mwanamke mwenye mzunguko mfupi wa hedhi wa siku 21 hupata ovulation siku ya 7, na uwezekano wa kupata ujauzito upo kuanzia siku ya 3 ya hedhi hadi siku ya 8 ya hedhi.
Hii inatoa maana kuwa wakati hedhi inaendelea (siku ya 3) tayari mwanamke husika anakuwa yupo kwenye siku za hatari. Pia, wanawake wenye mizunguko mifupi ya siku 22 hadi 24 wanaweza kupata mimba wakiwa bado wapo kwenye siku zao za hedhi.
Hivyo, kwa wanawake wenye mizunguko mifupi ya hedhi wanaweza kupata ujauzito wakiwa bado wapo kwenye kipindi cha kutoa damu za hedhi ikiwa watashiriki tendo la ndoa bila kutumia kinga.
"Ikiwa una mzunguko mfupi zaidi, mfano ule wa siku 21 hadi 24, hiyo inamaanisha kuwa una ovulation mapema katika mzunguko. Kwa sababu mbegu za kiume zinaweza kuishi ndani yako kwa hadi siku 5, unaweza kujamiiana mwishoni mwa kipindi chako na kisha kutunga mimba siku 4 au 5 baadaye sababu ovulation yako huja mapema.
Uwezekano wa kupata mimba wakati wa kipindi cha hedhi ni mdogo, lakini upo." inaandika taasisi ya American Pregnancy Association.
Utambuzi wa siku za Ovulation
Kipindi hiki hutawaliwa na mabadiliko makubwa ya kimwili na kihisia.
Dalili za uwepo wa hali hii hutofautiana miongoni mwa wanawake, baadhi yao huwa hawawezi hata kuhisi mabadiliko haya.
Muonekano wa yai siku ya ovulation
Kwa mujibu wa Tovuti ya Afyainfo, baadhi ya dalili zinazoweza kutumika kutambua siku hizi ni
- Ute wa mlango wa kizazi huzalishwa kwa wingi wakati huu, hufanana na ute wa yai la kuku lililopasuliwa.
- Mlango wa kizazi huongezeka ulaini wake, hupanda juu kidogo, hupanuka kiasi na huwa mbichi sana.
- Kuongezeka kwa hamu ya kushiriki tendo la ndoa.
- Maumivu ya nyonga.
- Kuwasha na kuvimba kwa matiti.
- Kuongezeka kwa uwezo wa kunusa na kutofautisha harufu mbalimbali za vitu.
- Sehemu ya nje ya uke (mashavu) au uke wenyewe kuonekana umevimba.