Nasikia Mzee Mwinyi ilibidi atoke hivyo hivyo bila kujiandaa lakini siku anatoka pale nyumbani alizuiwa na Mzee Natepe kuchukua mabati na mifuko ya simenti aliyokuwa amenunua kwa pesa zake mwenyewe kwa ajili ya ujenzi wa nyumba binafsi. Natepe alimkatalia kuvichukua akidai ni mali ya Serikali. Kweli Mzee Mwinyi akaviacha akaondoka.
Baada ya miaka kadhaa tu Mzee Mwinyi akateuliwa kuwa Rais wa Zanzibar na baadaye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Inadaiwa Mzee Natepe akajua kibarua kinaota nyasi lakini wakati Mzee Mwinyi anateua Baraza la Mawaziri akamteua tena Natepe kuwa Waziri pale pale mambo ya ndani.
- Tunachokijua
- Alhaj Ali Hassan Mwinyi ni Rais Mstaafu aliyeongoza Serikali ya awamu ya Pili. Aliingia madarakani Novemba 5, 1985 akichukua nafasi ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Alizaliwa Kivule, Mkuranga, mkoa wa Pwani mnamo Mei 5, 1925.
Kisiasa, Ali Hassan Mwinyi alijiunga na chama cha Afro Shiraz (ASP) mwaka 1964 na kushika nyadhifa mbali mbali za Serikali ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama vile katibu mkuu, Wizara ya Elimu Zanzibar 1963, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 1970 na kati ya mwaka 1982 hadi 1983 alikuwa Waziri wa Afya, Wizara ya Mambo ya Ndani, Maliasili na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Misri.
Mwaka 1984 alichaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mwaka 1985-1995 kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Madai ya kuzuiwa kuchukua baadhi ya mali zake baada ya kujiuzulu
Mwaka 1976 akiwa Waziri wa Mambo ya ndani, Mwinyi alilazimika kujiuzulu nafasi yake baada ya kutokea kwa mauaji katika mkoa wa Shinyanga na Mwanza yanayotajwa kufanywa na Polisi.
Inadaiwa kuwa baada ya kujiuzulu, nafasi yake kuchukuliwa na Mzee Natepe. Natepe alipoingia tu ofisini alimtaka Waziri Mzee Mwinyi kutoka katika nyumba ya Waziri arudi kwao Zanzibar ili yeye aweze kuishi hapo kama Waziri. Ilikuwa shida kidogo maana Mzee Mwinyi bado alikuwa anatafuta makazi lakini alitakiwa haraka kutoka.
Mzee Mwinyi ilibidi atoke hivyo hivyo bila kujiandaa lakini siku anatoka pale nyumbani alizuiwa na Mzee Natepe kuchukua mabati na mifuko ya simenti aliyokuwa amenunua kwa pesa zake mwenyewe kwa ajili ya ujenzi wa nyumba binafsi. Natepe alimkatalia kuvichukua akidai ni mali ya Serikali. Kweli Mzee Mwinyi akaviacha akaondoka.
Madai haya yalichapishwa pia JamiiForums Julai 23, 2019 kwenye uzi wenye kichwa cha habari "Jinsi Natepe alivyomhenyesha Rais Ali Hassan Mwinyi"
Aidha, inadaiwa kuwa baada ya Mwinyi kuwa Rais, Mzee Natepe aliogopa sana kuwa atafukuzwa kazi na kwamba Mzee Mwinyi baada tu ya kuapishwa kuwa Rais wa JMT wakati anateua baraza la Mawaziri akamteua tena Natepe kuwa Waziri palepale Mambo ya Ndani.
Ukweli wa madai haya upoje?
JamiiCheck imefuatilia madai haya na kubaini kuwa yana ukweli, lakini aliyemfanyia kitendo hiki ni Jackson Muvangila Makwetta na siyo Natepe kama mtoa hoja alivyodai.
Pia, tukio hili halikutokea baada ya yeye kujiuzulu Uwaziri wa Mambo ya Ndani mwaka 1976 bali lilitokea baada ya yeye kuhamia Zanzibar alipoteuliwa kwenye nafasi ya Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais anayeshughuliki mambo ya Muungano mwaka 1970.
Baadhi ya hoja zinazothibitisha ukweli huu ni hizi;
Kwanza, kwa mujibu wa taarifa rasmi za Wizara ya Mambo ya ndani, Waziri aliyefuata baada ya kujiuzulu kwa Ali Hassan Mwinyi ni Hassan N. Moyo (1977-1978) badala ya Abdalla Natepe kama inavyodaiwa. Baada ya Moyo, Salmin A. Juma (1979-1980) alishika wadhifa huo akifuatiwa na Abdalla Natepe.
Hii inathibitisha kuwa mtu aliyefuata baada ya kujiuzulu kwa Mwinyi sio Natepe kama inavyodaiwa, bali ni Hassan N. Moyo.
Aidha, yeye mwenyewe amefafanua kwenye kitabu chake 'Mzee Rukhsa'. Kwa maneno yake, Mzee Mwinyi anasema;
Baada ya muda nikateuliwa kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii. Baadaye tena nikabadilishwa na kuteuliwa kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Muungano. Ofisi ya wizara hiyo ilikuwa Zanzibar hivyo ilinilazimu kuhamia Zanzibar.
Wakati napata uhamisho huo nilikuwa nimeanza ujenzi wa nyumba yangu ninamoishi sasa hapa Mikocheni. Pale Oysterbay kwenye nyumba ya Serikali nilimokuwa naishi kulikuwa na vifaa vyangu vya ujenzi kiwemo nondo na matofali. Baada ya mabadiliko kwenye Baraza la Mawaziri nyumba ile alipangiwa Mh. Jackson Makweta aliyeteuliwa kuwa Waziri. Basi hakuwa na subira kunipa muda wa kuhamisha vifaa vyangu vya ujenzi, akaja nyumbani na kunitaka nimpishe mara moja na kusema niende kwetu Zanzibar.
Sikutaka ugomvi nikajiondokea na kumwachia nyumba pamoja na vifaa vyangu vya ujenzi. Akavichukua na mimi sikumdai, nina uhakika hii ilimsumbua sana. Na baadaye nilipokuja kuwa Rais tena bila kinyongo nikaendelea kumpa Uwaziri.
Hivyo, ni kweli Mzee Mwinyi alikutana na kadhia hii, lakini mtu aliyehusika Jackson Makwetta na siyo Abdalla Said Natepe kama mtoa hoja alivyobainisha.