Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Tabora imemhukumu aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Tabora mjini, Komanya Kitwala kumlipa fidia ya shilingi milioni 80 Alexander Ntonge mkazi wa kata ya Ipuli Tabora mjini, baada ya kupatikana na hatia katika mashitaka aliyofunguliwa ya kuwaamuru Askari Polisi kumkamata Ntonge na kumdhalilisha isivyo halali.
Akisoma hukumu hiyo katika shauri la madai namba 4 la mwaka 2021, Hakimu Mkazi, Jovith Kato alisema, mahakama imepitia ushahidi wa pande zote mbili na kujiridhisha kwamba Komanya Kitwala alitenda kosa hilo Januari 5 mwaka 2020, na hivyo mahakama imemuhukumu kulipa shilingi milioni 80 badala ya shilingi milion 140 ambazo mlalamikaji alidai kulipwa kutokana na makosa ya udhalilishaji.
Awali, wakili wa mlalamikaji, Kelvin Kayaga aliiambia mahakama kuwa, Komanya Kitwala alikwenda nyumbani kwa mlalamikaji akiwa na Askari Polisi ambao aliwaamuru kumkamata na kumtesa, kisha kumuweka ndani katika Kituo Kikubwa cha Polisi Tabora mjini bila kuwa na kosa lolote, ambapo baadaye aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora kwa wakati huo, ACP Safia Jongo aliagiza mlalamikaji Alexander Ntonge kuachiliwa huru kwa madai kulikuwa hakuna kosa lolote alilofanya.