Kwa Nini Utapeli Hauwezi Kuisha Na Jinsi Ya Kuepuka Kutapeliwa Kwenye Kujenga Utajiri

Makirita Amani

JF-Expert Member
Jun 6, 2012
1,915
3,407
Habari njema Matajiri Wawekezaji,

Karibuni kwenye mfululizo wa masomo yetu ya programu ya NGUVU YA BUKU, ambapo tunajifunza na kufanya uwekezaji kwa hatua ndogo ndogo na kujenga utajiri kwa uhakika.

Kauli mbiu yetu kwenye NGUVU YA BUKU, ambayo pia ndiyo imani yetu ni KILA MTU ANAWEZA KUWA TAJIRI. Hilo tuna uhakika nalo kwa sababu kwa fedha ndogo ndogo ambazo kila mtu anazipata, tukiziwekeza kwa muda mrefu kwa msimamo bila kuacha, tunaweza kujenga utajiri mkubwa.

Kwenye eneo la fedha na uwekezaji kumekuwa na utapeli mwingi sana unaoendelea. Kila mara huwa zinajitokeza fursa za kuingiza kipato na kuwekeza, ambazo zinaonyesha kuwa na manufaa makubwa. Lakini matokeo ya fursa hizo nyingi huwa ni utapeli unaopelekea wengi kupoteza fedha zao.

Watu wamekuwa wanalalamika kwamba kinachowazuia kuwekeza ni kuogopa utapeli, lakini hilo siyo kweli. Ukweli ni kinachowafanya wengi kutapeliwa ni kwa sababu hawataki kuwekeza.


Iko hivi rafiki, mtu akiambiwa kuhusu uwekezaji, swali la kwanza analouliza ni faida kiasi gani anapata? Akijibiwa faida atakayopata ni wastani wa asilimia 10 kwa mwaka mzima, anaona ni ndogo kwake kufanya uwekezaji.

Majadiliano ya aina hii yamekuwa yanajirudia mara nyingi kwenye mafunzo na ushauri wa uwekezaji;

Mshauri; “Wekeza eneo hili, lina hatari ndogo na faida nzuri.”

Mshauriwa; “Nikiweka milioni 10 naweza kupata faida ya kiasi gani kwa mwezi?”

Mshauri; “Wastani wa kama laki moja hivi.”

Mshauriwa; “Haa, yaani milioni 10 yote nipate laki moja tu! Si bora nikazungushe hiyo pesa mahali pengine nipate faida kubwa zaidi?”

Mtu huyo huyo anayekataa kuwekeza kwa sababu ya faida ndogo, haichukui muda unawakuta kwenye mazungumzo mengine ya aina hii;

Tapeli; “Ukiweka hela yako hapa, unapata mara mbili ndani ya mwaka mmoja kwa uhakika.”

Mtapeliwa; “Nikiweka milioni 10 naweza kupata faida ya kiasi gani kwa mwezi?”

Tapeli; “Kila mwezi unapata faida ya milioni 1 kwa uhakika.”

Mtapeliwa; “Hizo pesa natuma wapi? Nataka kuwekeza sasa hivi nisipoteze hiyo fursa.”

Na hivyo ndivyo mtu anaishia kutapeliwa, siyo kwa sababu alikubali kuwekeza, bali kwa sababu alikataa kuwekeza. Watu wengi wenye fedha ambazo wanaishia kutapeliwa, tayari ni watu ambao wanajua kuhusu uwekezaji, lakini kwa sababu hawataki kuwekeza, wanaishia kutapeliwa.

KWA NINI UTAPELI HAUWEZI KUISHA.

Utapeli hauwezi kuisha kwa sababu ya tamaa ya watu kutaka kupata faida kubwa na kwa haraka bila ya kufanya kazi ngumu. Haya ni matamanio ambayo yamekuwepo tangu enzi na enzi na aina zote za utapeli huwa zinaanzia hapo.

Matapeli wote wanajua jinsi ya kucheza na saikolojia ya binadamu, kwa sababu wanajua tamaa ambayo watu wanayo, huwa wanakuja na mipango inayoamsha tamaa hiyo na kujinufaisha.

Maendeleo ya teknolojia tunayopitia sasa yamewachanganya wengi na kupelekea utapeli kuwa mkubwa zaidi. Kumekuwa kunakuja teknolojia mpya ambazo watu hawazielewi, lakini zinaonekana kuwa na faida kubwa na hivyo watu kushawishika kuwekeza.

Kwa kuwa watu hawana uelewa wa kutosha juu ya teknolojia hizo mpya na kwa sababu wengi wanakimbilia kuwekeza, nao wanafuata mkumbo ili wasipitwe.

Hivyo ndivyo teknolojia mpya kama sarafu za kidijitali (Crypocurrency) zimetumika kuwatapeli watu wengi. Teknolojia ni sahihi, lakini ile faida kubwa ambayo wengi wanashawishiwa wataipata siyo sahihi. Ukuaji wa haraka wa thamani ya hizo sarafu za kidijitali haimaanishi ni uwekezaji sahihi, zaidi inaonyesha jinsi tamaa za watu zinavyoweza kuwapoteza.

Kwa mwenendo huu wa maendeleo ya teknolojia kutokueleweka vizuri, huku tamaa ya watu kunufaika bila gharama ikiwa kubwa, utapeli hauwezi kuisha.

JINSI YA KUEPUKA KUTAPELIWA KWENYE KUJENGA UTAJIRI.

Tumeona hapo juu kwa nini utapeli hauwezi kuisha, swali ni je hakuna namna kuepuka kutapeliwa? Jibu ni njia zipo na kwenye programu yetu ya NGUVU YA BUKU tuna njia ya uhakika.

Njia ya kuepuka kutapeliwa kwenye kujenga utajiri inahusisha hatua mbili; KIPATO na UWEKEZAJI.

Kwenye kipato ni kuhakikisha unakuwa na njia za uhakika za kuingiza kipato ambazo zinatoa thamani kwa watu wengine. Shughuli yoyote ya kukuingiza kipato unayoifanya, swali la kwanza unalopaswa kujiuliza ni thamani gani unayoitoa kwa wengine. Ni tatizo gani ambalo watu wanalo na unalitatua au mahitaji gani wanayo na unayatimiza. Epuka sana njia za kuingiza kipato ambazo zinaahidi kuingiza kipato kikubwa huku ikiwa haionyeshi wazi ni thamani gani inayotolewa.

Kwenye uwekezaji ni kuhakikisha unawekeza maeneo sahihi ambapo uwekezaji huo unatumika kwenye shughuli sahihi za kiuchumi na kuzalisha faida kwa namna inayoonekana wazi. Epuka sana uwekezaji ambao unaahidi faida kubwa lakini haionekani wazi hiyo faida inazalishwaje.

Kwenye kuchagua uwekezaji sahihi, angalia mambo haya matatu;

1. Shughuli iliyo nyuma ya uwekezaji unaofanya. Uwekezaji huwa unaenda kukuza shughuli ambazo tayari zinaendelea, uwekezaji sahihi ni ule unaofanywa kwenye shughuli sahihi. Kama huwezi kuelezea uwekezaji wako unazalishaje faida kwenye shughuli zinazofanywa, jua siyo uwekezaji sahihi na kuna hatari ya kutapeliwa.

2. Muda ambao uwekezaji huo umekuwepo. Kama kitu kimedumu kwa muda mrefu, ni kiashiria kwamba kipo sahihi. Vitu vingi visivyokuwa sahihi huwa vinavuma kwa muda mfupi na kupotea. Kwenye uwekezaji huwa zinakuja fursa zinazoonekana ni nzuri, lakini baada ya muda mfupi zinapotea. Fanya uwekezaji kwenye vitu ambavyo vimedumu kwa muda mrefu na utaepuka kutapeliwa. Hili ni gumu kwa sababu watu huwa wanahamasishwa wachangamkie fursa kabla haijajulikana na wengi, na hapo ndipo wanapopigwa vizuri. Ni bora ukose faida kubwa kwa kuchelewa kuwekeza kuliko ukimbilie kuwekeza na upoteze kila kitu.

3. Linganisha mwenendo wa uchumi na faida inayonadiwa kwenye uwekezaji. Mwenendo wa uchumi huwa unaakisiwa na viwango vya riba vinavyowekwa na benki kuu na benki za biashara. Kwa wastani riba zinazotozwa na mabenki ni asilimia 20 kwa mwaka. Hicho ndiyo kiashiria cha mwenendo wa uchumi. Sasa unapokuja kuahidiwa uwekezaji unaozalisha asilimia 100 kwa mwaka, unapaswa kuwa na wasiwasi ni kwa uchumi gani hiyo faida kubwa kiasi hicho inazalishwa. Ni kweli zipo biashara na shughuli ambazo zinazalisha faida kubwa, lakini siyo nyingi wala rahisi kama inavyochukuliwa na watu. Hivyo kuwa upande salama na kuepuka utapeli, epuka uwekezaji unaoahidi faida kubwa kuliko viwango vya kiuchumi. Kwa sababu hata kama upo, watu hawatakuwa na muda wa kuja kukubembeleza uwekeze, kwani watakuwa ‘bize’ sana kuvuna hizo faida kubwa.

Kwa zama tunazoishi sasa, utapeli umekuwa mwingi na mgumu sana kujua. Njia pekee ya kuepuka kutapeliwa ni kuwa mwekezaji makini na kuwekeza kwa usahihi.

Karibu kwenye SEMINA YA KISIMA CHA MAARIFA 2024 ambapo utakwenda kujifunza na kuweka mpango huu kwa vitendo kisha kusimamiwa kwenye kuutekeleza kwa msimamo bila kuacha. Tuma sasa ujumbe wenye maneno SEMINA 2024 kwenda namba 0713 604 101 upate nafasi ya kushiriki semina.

SIKILIZA SOMO HILI KWENYE ONGEA NA KOCHA.

Kwenye kipindi cha ONGEA NA KOCHA tumekuwa na mjadala mzuri wa somo hili ambapo washiriki wamekuwa na maswali na michango mbalimbali. Karibu usikilize hapo chini ili ujifunze na kuchukua hatua sahihi.


View: https://youtu.be/R6FykHbs57I

MJADALA WA SOMO.

Karibu kwenye mjadala wa somo hili, shiriki kwa kutuma majibu ya maswali haya;

1. Kwa nini utapeli hauwezi kuisha?
2. Ni kwa jinsi gani tunaweza kuepuka kutapeliwa kwenye kujenga utajiri?

3. Unatumiaje shughuli ya uwekezaji kupima usahihi wa uwekezaji?

4. Unatumiaje muda kupima usahihi wa uwekezaji?

5. Unatumiaje mwenendo wa uchumi kupima usahihi wa uwekezaji?

6. Unaitumiaje programu hii ya NGUVU YA BUKU kuepuka kutapeliwa?

7. Karibu kwa maswali, maoni, mapendekezo na shuhuda kuhusu somo hili na programu nzima ya NGUVU YA BUKU na UHURU WA KIFEDHA.

Tuma majibu ya maswali hayo kama uthibitisho wa kusoma, kuelewa na kutekeleza somo hili la uwekezaji.

Nenda kayaweke haya uliyojifunza kwenye matendo ili uweze kujenga mafanikio makubwa kwenye maisha yako kwa kuiishi kila siku yako kwa mafanikio makubwa.

Kutoka kwa rafiki yako anayekupenda na kukujali sana,

Kocha Dr. Makirita Amani,

Daktari |Mwandishi |Kocha |Mkufunzi

+255 678 977 007 / amakirita@gmail.com

www.amkamtanzania.com

MUHIMU; Rafiki, nikushukuru kwa kuendelea pamoja kupitia mafunzo haya ninayotoa. Karibu kwenye huduma zaidi ninazotoa, kuanzia 1. VITABU, 2. NGUVU YA BUKU, 3. KISIMA CHA MAARIFA, 4. CHUO CHA MAUZO na 5. BILIONEA MAFUNZONI. Kupata maelezo ya huduma hizi, tumia mawasiliano yaliyopo hapo juu. Karibu sana.
 
Back
Top Bottom